Mada za sehemu hiiUhakiki Wa Kazi Za Fasihi AndishiMada 4
- Uhakiki wa ushairi
- Uhakiki wa riwaya
- Uhakiki wa tamthiliya
- Uhakiki wa diwani
UHAKIKI-TAMTHILIA KITABU: NGUZO MAMA
MWANDISHI: PENINA MHANDO
MWACHAPATI: DUP
MWAKA: 1982
Tamthiliya inazungumzia matatizo mbalimbali yanayowakabili wanawake katika jamii ya kitanzania na afrika kwa ujumla. Mwandishi anaonesha unyanyasaji na mateso ya wanawake kutoka kwa waume zao kutokana na mfumo dume uliojengeka katika jamii nyingi.ametumia mandhari ya patata kuyasawiri maisha ya mwanamke wa kiafrika.
Ukombozi wa Mwanamke
Ni tamthiliya inayochambua kwa undani matatizo mbalimbali yanayowakabili wanawake pamoja na jitihada zao ili kujikwamua katika minyororo ya utumwa kwa mwanaume na manyanyaso mengine mazito mengine wanayoyapata kutoka kwa jamii kwa ujumla. Ameyataja manyanyaso hayo kama vile: wanawake kupigwa, kufanyishwa kazi nyingi (kufua, kupika, kulea watoto, kuchota maji, kukusanya kuni n.k). Pia ameonesha mbinu mbalimbali zinazoweza kutumiwa na mwanamke kujikomboa. Mwandishi ameugawa ukombozi wa mwanamke, kama ifuatavyo
Ukombozi wa Kiuchumi
Mwandishi kwa kuwatumia wanawake wa patata ameonesha jinsi walivyoanzisha miradi ambayo ingewawezesha kujipatia fedha na kuwafanya wanawake wote wajitegemee, Wasiwe tegemezi.
"BI NNE Miradi tutatiliya mkaazo, Miradi Yakila aina, vilabu vya pombe, maduka Ya kanga, ushirika wa kushona, kupika Hotel na mengine mengi… "
BI PILI naye aliamua kuanzisha kilabu cha pombe ili aweze kujikwamua katika maisha magumu kiuchumi.
"BI MSIMULIZI Kaamua bi pili
Pombe kujipikia na kilabuni Kuiuza, pesa akipata, pesa msema Kweli. Na mauzo mama atasimama" Nukuu hii inonesha umuhimu wa pesa katika ukombozi wa mwanamke, kwani pesa ndiyo iletayo maendeleo stahiki.
Bi moja alijiunga na wenzake na kuanzisha viwanda vya kufuma mapambo ya nyumbani.
"BI MSIMULIZI katokea bi moja Na wazo lake jipya kiwanda Kuanzisha mapambo ya nyumbani Kufuma "
Ukombozi Kijamii
Kwa kutumia mhusika bi Nane mwandishi amonesha ukombozi wa kijamii kwani alianzisha umoja wa walimu wa kike, Lengo likiwa kutatua matatizo mbalimbali yanayowakabili katika ufundishaji.
"BI MSIMULIZI katokea bi nane na wenzake
Wengi makubwa hawakujitakia Vizuri walijishauri
Tuanze na yetu matatizo………..
Kazi yetu yakufunza vyema kuchapa Vingi vikitokomea
Vyema vijana watafunzika"
Mwandishi anaonesha kuwa elimu ni nyenzo mojawapo ya kumkomboa mwanamke, Katika kumkomboa mwanamke kijamii, mwandishi ameonesha jamii nzima lazima ishirikishwe, Mwanamke peke yake atoweza kujikomboa.
"BI NANE……tushirikishe wanaume pia
Nguzo mama inafaida kwa wote"
Mwandishi anaonesha mwanamke akikomboka ni faida kwa jamii nzima. Pia mwandishi anaonesha umoja na mshikamano kama njia itakayowawezesha wanawake kujikomboa.
Pia mwandishi anaonesha kupitia mikutano watu wengi wataelewa zaidi kuhusu ukombozi wa mwanamke na …, wayapatayo wanawake nahivyo kuwa rahisi kubadilika.
Ukombozi wa Kisiasa
Mwandishi anaonesha juhudi mbalimbali za wanawake wa patata ili kujikomboa kisiasa. Nafasi za uongozi kwa wanawake ni moja kati ya njia hizo ndiyo maana mwandishi anonesha jitihada mbalimbali zilizofanywa na wanawake wa patata ili kuchukua uongozi serikalini. Mwandishi anasema:
"BI NNE madaraka kwa akina mama Jambo hili tumetilia mkazo, Wakina mama watapewa vyeo Orodha tumeshapanga, tutapata Mawaziri, mameneja, mabalozi n.k Wengine tayari wameshapata kama Tunavyofahamu" Mwaandishi ameonesha umuhimu wa mwanamke kupewa uongozi kujikomboa kisiasa. Baadhi ya waliopata uongozi ni Bi Nne, mwenyekiti wa kamati ya vyeo. Bi Tatu, mwenyekiti wa kamati ya malezi bora. Bi Nane mwenyekiti wa umoja wa walimu.
Ukombozi wa Kifikra
Mwandishi ameonesha tatizo linalosumbua wanawake wengi, Wanawake wengi wamekuwa na fikra potofu. Kuwa baadhi ya mambo ni ya wanaume tu hayamuhusu mwanamke, mfano , uongozi , kufanya kazi , kumiliki njia za uzalishaji mali , kujitegemea wao wenyewe n.k kwa mfano bi Nne aliyekuwa mwenyekiti wa wanawake alishiriki kuyachunguza mashtaka ya bi Nane na akatoa hukumu kwa kusikiliza upande mmoja, jambo hili ni fikra potofu. Bi Nane licha ya kufahamu kuwa mashtaka yake ni ya uongo anakubali kila kitu alichoelezwa na bi Nne.
Kwa ujumla ukombozi wa kifikra juu ya wanawake na jamii kwa ujumla vinahitajika ili kufikia ukombozi wa kweli wa mwanamke.
Uongozi Mbaya
Mwandishi ameonesha umuhimu wa uongozi katika jamii. Pia amemuonesha kiongozi kama mtu anayeweza kuipeleka jamii katika mafanikio, au katika matatizo.
Mwandishi anasema:
"BI NNE' tena kwetu sie kiongozi uongeza njia
Aweza kutupeleka kwenye neema
Au mdomoni mwa simba"
Viongozi wengi wamekuwa wakipelekea jamii zao katika midomo ya simba, kwani hutumia uongozi wao kujipendelea wenyewe, na kujiona watukufu kwenye daraja la juu, Wanafanya maamuzi watakavyo bila kufuata utaratibu. Mwandishi anasema:
"BI MSIMULIZI: bi Nane akawaza kumbe kazi Hii ya uongozi au uwenyekiti Inampa mtu uwezo wa kufanya Mambo kinyume cha kawaida" Kutokana na dondoo hizi mwandishi anathibitisha kuwa uongozi mbovu ndio chanzo cha matatizo yanayoikabili jamii ya patata. Viongozi kama bi Nne na mwenyekiti wa kamati mashauri, mfano wa viongozi wabovu wanaorudisha nyuma.
Udikteta umeoneshwa kama tatizo linalotokana na uongozi mbovu. Kiongozi kama mwenyekiti wa kamati ya mashauri ameoneshwa kama dikteta anayetumia uongozi atakavyo. Anaongozwa na hisia au kufuata anavyoambiwa na watu wengine wa karibu badala ya kufuata miongozo ya kikatiba iliyowekwa. Mwenyekiti anatumia vitisho kumlazimisha bi Nne akubaliane na kitu ambacho ajafanya kwakuwa yeye ni kiongozi, pia anaamua kesi kwa kusikiliza upande mmoja bila kumpa mshitakiwa nafasi ya kujieleza. Mwandishi anasema:
"BI MSIMULIZI: vipi mtu atatoa ushauri
Kufuatia maelezo ya mshitakiwa pekeyake
Tena tuliyoelezwa wakati mshitakiwa hakuwepo?
.............................................................................
Na ajabu kupita yote
Vipi mwenyekiti bila kamati Akatoa ushauri katika mashtaka?"
Pia baadhi ya wanawake utumia madaraka ya waume zao ili kuwakandamiza wenzao, na hivyo kukwamisha harakati za ukombozi wa mwanamke.
Mfano: bi tatu anasema.
"mkitaka nitalipa hela badala ya Kufanya kazi samahani, kwaherini Tena hata kesho siwezi kufika, Tuna Pati nyumbani kwetu ya kazini kwa Mume wangu kwahiyo sitafika"
"BI NANE: haya jamani sisi tusiokuwa na Wanaume wa kutubembeleza sisi ambao Waume zetu sisi watu wakubwa tuendelee"
Katika hali halisi wanawake baadhi, hutumia madaraka ya waume zao kunyanyasa wanawake wengine badala ya kuyatumia kuwaakomboa, Pia mwandishi anaonsha kuwa viongoziwaliopewa madaraka na waliotegemewa kufanya mabadiliko ndiyo wamekuwa viongozi wabovu. Mfano
"kwa wema na kwa huruma Labda kamuelezea bi Nne"
Chizi anamshangaa bi Saba kwani licha ya kuudhuria vikao mbalilmbali alikuwa aelewi hata nini maana ya NGUZO MAMA na pia viongozi hawakuweza kumsaidia kwa lolote.
Elimu
Elimu imeoneshwa kama nyenzo muhimu katika mandeleo ya jamii. Mwandishi wa tamthiliya hii amethibitisha umuhimu wa elimu katika ukombozi wa mwanamke na jamii kwa ujumla. Mwandishi anasema.
"BI NNE: tumepiga nia sana,
: Jambo hili la ushonaji, sasa tutapata vitu
: Patata kate. Pia somo laushonaji, litatiliwa
: Mkazo mashuleni. Kila shule itafundisha ili
: Watoto wetu wajue kushona, wavae vizuri na
: Kupamba nyumba zao vizuri".
Kwa upande mwingine bi Nane anaonesha kuwa watu wasipopata elimu hawatapata maendeleo pia.
"BI MSIMULIZI…………………………
Tuvitoe vigingi vile vituzuiavyo,
Kazi yetu ya kufunza vyema kuichapa Vigingi vikitokomea
Vyema vijana watafunzika Wakifunzika wote patata NGUZO MAMA Itasimama".
Dondoo inatuonesha kuwa kutokana na kukosekana kwa elimu jamii ya patata imeshindwa kupata maendeleo na kuwakomboa wanawake.
Pia elimu imeoneshwa kama kikwazo cha uongozi. Viongozi hawakuwa na elimu kiasi kwamba hawakujua kinachoendelea katika masuala ya uongozi. Kwa mfano: bi Nne alikuwa na uongozi mbaya kwasababu hakuwa na elimu. Pia wakina mama wengi hawakufahamu masuala ya uongozi na hata viongozi wao kutokana na kutokuwa na elimu, Wala viongozi wake. Baada ya chizi kumuuliza bi Saba, anajibu hivi:
"BI SABA………..
Mwanangu mie sijui, Labda kamuulize bi Nne
Lakini juzi kachaguliwa katibu Sijui na kamati gani ile, nimesahau"
Kwa upande mwingine mwandishi amezungumzia umuhimu wa elimu ya malezi katika jamii. Katika ulimwengu wa sasa ambao unakabiliwa na matatizo mengi, kama vile magonjwa (UKIMWI), tamaa ya pesa, matumizi
ya dawa za kulevya na kuporomoka kwa maadili kwa kiasi kikubwa, elimu ya malezi inaonekana kuwa ya muhimu zaidi katika jamii.
Mwandishi anasisitiza kuwapo kwa elimu ya malezi itakayo wasaidia vijana na wanawake hasa wale wanaokumbana na matatizo mbalimbali kama vile utoji wa mimba na kutupa watoto sharti wapate elimu ya malezi ili waache tabia hiyo.
"BI NNE: pia wasichana kutupa
watoto kwenye mapipa kuna semina wiki ijayo kuzungumzia jambo hili ni aibu kubwa sana kwetu"
Sambamba na hilo mwandishi anataka elimu ya malezi itolewe pia kwa jamii ili ukombozi wa kweli upatikane. Mfano, mwandishi anaitaka jamii ielimishwe ili kubadilisha sheria ya ndoa. Kila mtu awe na mke mmoja, Pia itungwe sheria ya kuwabana wanaume wanao piga wake zao ovyo. Mwandishi anasisitiza kuwa elimu itolewe kwa watu wakubwa wenye tabia ya kuwapa mimba watoto wa shule, Pia itungwe sheria kalli itakayodhibiti tabia hiyo.
"BI NNE: sheria ya ndoa itabadilishwa
Kila mtu mke mmoja……..
Na mambo ya kupigwapigwa hatutaki Pia mabo ya watoto wa shule kupewa Mimba ovyo, Tene na watu wakubwa
Kwa miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia mmomonyoko mkubwa katika jamii yetu,Hivyo elimu ya malezi bora ni muhimu sana kwa ustawi wa jamii.
Dhuluma
Mwandishi amemtumia Bi Saba kuonesha jinsi wananwake wengi wa kiafrika wanavyodhulumiwa mali, hasa wajane, pindi wanapofiwa na waume
zao. Bi Saba baada ya kufiwa na mume wake alidhulumiwa mali zote alizochuma na mume wake. Shemeji zake waligawana kila kitu hadi watoto na kumuacha bi saba akihangaika asijue la kufanya.
"BI SABA………..hao! Shemeji mmerudi kuchukua hata
Kitanda! Hata sufuria! Nitalala wapi
Na nitapikia wapi jamani!"
Mwandishi ameonesha wanawake wengi wanao dhulumiwa hawana msaada ndiyo maana dhuluma imetapakaa kila mhali.
"BI MSIMULIZI…………………………
Akalia bi Saba tena akalia Hana wakumsaidia
Mumewe kafa nduguze wanakuja juu Vyombo na nguo zote wakagawana
.............................................................................
Kiti hiki changu, mie lile jembe,
Mie suruali hizi, ilimradi likawa zogo"
Dondoo hii inathibitisha kuwa dhuluma ni tatizo lililopo katika jamii yetu.
Kwa upande mwingine mwandishi ameonesha dhuluma inayofanywa na viongozi dhidi ya wale wanaowaongoza. Viongozi wanaonekana kupewa kipaumbele zaidi katika mambo mbalimbali kuliko wale wanao ongoza. Mfano chizi amemuonesha bi. Nne kuwa yeye ni mtu mkubwa na anayepewa kipaumbele zaidi.
"CHIZI……………………………..
Lakini bibi yangu aliniambia
Binadamu wote sawa"
Pia mwandishi anaonesha jinsi viongozi wanavyowadhulumu wanao waongoza kwa kuwalazimisha na kuwapa masharti yaliyo kinyume na katiba. Hii ni dhuluma dhidi ya democrasia.
"MWENYEKITI: Jambo la pili nakueleza kuwa Hakuna mtu yeyote anayeruhusiwa Kufanya mkutano bila kibali cha Ofisi hii ………………………………
Sheria hii ipi na inajulikana" "BI MSIMULIZI: lahaula!
Sheria hii bi nane hajapata kusikia"
Pia kitendo cha viongozi kutokuwajibika na baadhi hata kutofahamu maana ya NGUZO MAMA, ni dhuluma dhidi ya wale wanaowaongoza.
Usaliti
Mwandishi ametuonesha suala la usaliti kama tatizo linaloikabili jamii yetu. Mwandishi amonesha waalimu wenzao, Bi Nane kwa kutoa siri za vikao wanavyovifanya na kumpelekea bi nne ambaye ni adui wa bi nane. Usaliti huu ulimsabaishia matatizo bi nane kwani alituhumiwa kuwa ni msaliti na mvuruga amani. Mwandishi anasema;
"BI NNE …
Tena mwenyekiti mimi Nilikwambia hao walimu Wengine awampendi bi Nane
Yeye tu ndiye anayejiweka kimbelembele kama Anawapenda mbona wanatoka kueleza mipango yao?"
Pia usaliti huu ulipelekea bi Nane kuingia kwenye migogoro mikubwa na mwenyekiti
"MWENYEKITI………………………..
Kwa kifupi nikwamba tumepata habari Kwamba wewe umeanzisha kukindi cha Kupinga juhudi za wenzenu……………………
Tena kikundi hicho kimekuwa kikifanya Mikutano kupanga njama za kuchafua"
Kwa upande mwingine mwandishi ameonesha jinsi ambavyo baadhi ya watu huwaka kwa ndugu zao kutokana na matatizo waliyokuwa nayo. Mfano shangazi yake chizi alimkana tena huku akimdhiaki kwa kumtukana na kutaka kumuitia mbwa.
"CHIZI……………………………..
Huyu bi tatu ni shangazi yangu
Haki ya mungu tena! Naambiwa yeye Ni shangazi yangu kabisa katoka baba
Yangu alafu yeye. Siku moja… ngojeni
Niwaoneshe".
"BI TATU: usiniite shangazi. Toa balaa lako Hapa. Ukirudi nitakuitia mbwa
Akuume"
Dondoo hii inatuonesha jinsi jamii ilivyobadilika, wazazi ambao ni tegemeo la watoto, hawawathamini, hasa watoto wenye matatizo.
Pia usaliti wa mume wa bi Tano na bi Sita dhidi ya bi Tano.
Uvivu na Uzembe
Mwandishi ameonesha kuwa watu wa jamii ya patata ni wavivu na wazembe, yaani hawawajibiki ipasavyo katika kufanya kazi. Mwandishi ameonesha uvivu na uzembe umechangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha jitihada za akina mama katika kuinua nguzo mama. Mfano wakina mama walipokuwa wakiinua "NGUZO MAMA" baadhi walikuwa wanategea kwa kufanya mazungumzo ambayo ayakuhusiana na mukutadha wa kazi hiyo. Mwandishi anasema;
"BI NNE:
Haya bi Moja, bi Mbili, bi Tatu. Vuta!
Tena vuta!"
"BI MOJA: aise hizi kanga mpya umenunua wapi?" "BI TANO: huna habari kuwa zimetoka? Hizi Nimenunua jana pale kwa mwarabu"
"BI NANE: Sasa jamani bi moja una kwenda wapi tena?" "BI MOJA: Aaa, jamani nitarudi, lakini kanga hizi sikosi"
Pia mwandishi ammuonesha bi Sita kama mwanamke asiyewajibika kwani kwake wanaume ni muhimu kuliko kazi.
Bi Tatu naye anaacha kufanya kazi na kuamua kufuatana na mume wake kwenda kwenye sherehe kwani kwake yeye sherehe ni muhimu zaidi kuliko NGUZO MAMA". Mwandishi anasema.
"BI TATU: Sio utani ndugu yangu. Tunakwenda Kwenye pati na mume wangu leo saa moja lazima nipalilie unga kwa baba watoto wangu ati, Nitakula nini"
Viongozi nao wnaonekana wababaishaji, wamejaa maneno pasipo kuwajibika, Kwa mfano bi Nne ambaye ni kiongozi anaacha kazi ya kunyanyua NGUZO MAMA na kwenda kwenye vikao ambayo ni kazi ya kupiga soga.
Kutokuwajibika kwa viongozi pamoja na wanawake kwa ujumla unakwamisha harakati za kuinua NGUZO MAMA pia kwa kiasi kikubwa ugumu wa maisha katika jamii yetu unatokana na tabia ya uvivu na uzembe.
Mapenzi na Ndoa
Mwandishi ameyajadili mapenzi katika sura mbili, Kwanza ameonesha mapenzi yanayo jali pesa, usaliti pia katika mapenzi na ndoa. Amonesha mapenzi yanayojali pesa kwa kutumia maganga mume wa bi tano. Anamsaliti mkewe na kuwa na mahusihano na bi sita. Bi tano anasema:
"BI TANO: …
Wee bi sita mshenzi, Unanichukulia
Mume wangu hivihivi kimacho macho"
Usaliti huu unapelekea ugumu wa maisha kwa familia ya bi Tano, kwani watoto wanalala njaa kwa kukosa chakula na mahitaji mengine muhimu.
Pia mwandishi anaonesha jinsi mapenzi yanayoendeshwa na pesa badala ya utashi wa mtu. Mfano; mapenzi kati ya bi Tatu na mume wake yaliendeshwa na pesa.
"BI TATU…………………
Unasema hivyo kwakua wewe Unakazi ya mshahara hata Ukiachwa unajitegemea, na mie je
............................................................................. Tuna pati nyumbani kwetu ya Kazini kwa mume wangu kwa
Hiyo sita fika"
Kwa upande mwingine mwandishi ameonesha mapenzi ya uongo yanavyotawaliwa na misukosuko mingi. Mfano Sudi alikuwa akimpiga mara kwa mara bi Pili.
Hii inaonesha kwamba Sudi hakuwa na mapenzi ya dhati kwa mkewe.
"SUDI: Wacha mdomo nitakupiga mbele ya hawara zako"
Sambamba na hilo mwandishi anaonesha jinsi jamii inavyokubaliana na tabia ya wanaume kuwa na mke zaidi ya mmoja, Anaonesha jinsi wanawake wanavyojitahidi kulibadilisha suala hili.
Nafasi ya Mwanamke
Mwandishi amemchora mwanamke katika namna tofauti tofauti,
Kama chombo cha starehe. Ameoneshwa kwamba anatumia mwili wake kama bidhaa iuzwayo sokoni na kumpatia faida. Kwa mfano bi Sita alikuwa kahaba. Mwandishi anasema:
"BI MSIMULIZI:
Mji huu sikuingia leo ndugu Yangu, mawaziri makabwera Mapadri kwa mashehe vijana Kwa wazee, mie breki mie jeki Kwangu mie utasimama"
Bi Sita alitumika kama starehe ya mume wa bi Tano na hivyo kusababisha migogoro kati yake na bi Tano
-
Kama kiumbe duni asiyekuwana thamani wala uwezo wa kufanya jambo lolote katika jamii. Mwandishi ameonesha wanaume waliwadharau sana na kuwabeza wanawake na kuwaona watu wasiokuwa wakamilifu.
-
Kama jasiri mwenye kujitoa mhanga na mwenye elimu. Mfano Bi Nane alikuwa na elimu na alitumia vizuri kwa maendeleo ya jamii nzima. Pia alionesha ujasiri wake alipomjibu mwenyekiti kufuatia shitaka alilotakiwa kujibu kwani alitakiwa kujibu kwa maandishi.
-
Kama mtu mtumwa wa mwanaume, mwanamke ni chombo cha uzalishaji mali, mfano Bwana sudi alimtumikisha mkewe Bi pili na kumuachia majukumu ua kutafuta mahitaji ya familia huku yeye akiwa anakunywa pombe tu.
-
Kama kiongozi wa familia ambaye amebeba majukumu ya kuikuza jamii na kama mwanamke asingekuwepo katika jamii na jamii isingekuwepo.
Nafasi ya Mwanaume
- Amependelewa
- Mvivu mfano Sudi
- Muonevu mfano Sudi
- Chombo cha starehe mfano Maganga
- Kukosekana kwa umoja na mshikamano miongono mwa wanawake ni kikwazo kikubwa cha ukombozi wa wanawake.
- Ulevi, uvivu, unafiki na usaliti ni maadui wa maendeleo
- Ili tuweze kupata maendeleo ya kweli katika kila jambo ni lazima jamii nzima ishirikishwe.
- Uongozi ni jambo la msingi katika kufikia malengo mbalimbali tunayojiwekea
- Wanawake pia wanastahili kupewa nafasi za uongozi sawa na wanaume
- Suala la malezi kuwa ni muhimu katika familia na sharti lihusishe wazazi wote wawili
- Kuwa na mke zaidi ya mmoja ni kikwazo kwa familia na jamii kwa ujumla.
- Wanaume ni kikwazo cha ukombozi wa mwanamke hivyo wanahitaji kuelimishwa ili kiondokana na dhana potofu ya kuwaona wanawake kama viumbe duni wasioweza kuchangia chochote katika maendeleo ya jamii.
- i. Kati ya Bwana Sudi, Shaba, na Totolo. Chanzo ni shaba na Totolo kumtetea Bi Pili ambaye alikuwa mke wa Sudi. Suluhisho la mgogoro ni kwamba Bi Pili aliamua kukimbia.
- ii. Kati ya chizi na shangazi yake Bi Tatu, hakumpenda wala kumthamini Chizi na hiki ndicho chanzo cha mgogoro suluhisho ni kwamba Bi Tatu aliamua kumfukuza bila kumpa msaada wowote Chizi.
- iii. Kati ya Bi Saba na shemeji zake. Chanzo ni kifo cha mume wa Bi Saba. Baada ya kufiwa na ndugu wa mume wake waliamua kuchukua vitu vyote, hivyo kumtaka Bi Saba, lakini Bi Saba alikataa. Mwisho waliamua kumnyang'anya vitu hivyo kwa nguvu wakagawana mpaka watoto.
- iv. Kati ya Sudi na mkewe, Chanzo ni bwana Sudi kudai pesa kwa mkewe na mkewe akakataa kwani zilikuwa zinahitajika kwa familia nzima. Suluhisho ni kwamba Sudi aliamua kumpiga mkewe.
- v. Kati ya Bi Tano na Bi Sita. Chanzo Bi Sita kumchukua mume wa Bi Tano. Na suluhu ni Bi sita kuondoka na Bwana Sudi kukimbia.
- vi. Mgogoro kati ya Bi Tano na wanakikundi, chanzo ni vitambaa alivyopewa Bi Tano kutokuuzika. Suluhisho ni kwamba aliamua kugawana vitambaa kila mtu akauze.
- Mgogoro kati ya Bi Nne na Bi Nane.
- Mgogoro kati ya......................................
Msimamo wa mwandishi ni wa kimabadiliko kwani ameweza kuonesha matatizo mbalimbali yanayowakabili wanawake katika harakati za kujikomboa na kwa baadhi ya matatizo hayo ameeleza nini kifanyike.
Mtazamo wa mwandishi ni wa kiyakinifu kwani matatizo aliyoyaeleza dhidi ya wanawake ni halisi na yapo katika jamii yetu. Pia mbinu alizopendekeza kukabiliana na matatizo hayo ni mbinu sahihi.
Mwandishi anaamini kuwa ili wanawake waweze kujikwamua lazima wawe na maelewano umoja mshikamano kusiwepo na usaliti, pasiwepo na wivu wala kugombana.
Muundo
Mwandishi ametumia muundo msago yaani matukio yamepangwa toka mwanzo na kusimuliwa kwa mfululizo mpaka mwisho. Mwandishi amegawa tamthiliya katika maonesho manne ambayo katika onesho la kwanza ameanza kuonesha nguzo ikiwa chini na harakati za wanawake kuinua kuanzia onesho la pili mpaka la tatu anaonesha jitihada walizofanya akina mama kuinua nguzo mama na matatizo mbalimbali jinsi akina mama mbalimbli walivyokumbana nayo. Onesho la mwisho linaonesha jinsi akina mama walivyoshindwa kabisa kuinua NGUZO MAMA
Mtindo
Mwandishi ametumia mtindo wa dailojia na analojia kwa kiasi kikubwa.
"BI MSIMULIZI: kwa vile chizi kakimbia
Hadithi tamalizia Wakaamua wakainuka Siku ya kwanza ikapita NGUZO MAMA pale pale" "BI NNE: Inuaaa!
BI NNE: Hebu tutazame kwanza kwanini haisogei?"
Pia mwandishi ametumia lugha ya kishairi ili kuongeza mvuto katika kazi yake.
Mfano :
"CHIZI; Chizi mie chizi mie Sikizeni langu rimba Rimba nimelitengeneza Kwa mikono yangu hii"
Pia kuna matumizi ya hadithi ndani ya tamthiliya ambacho ni kipengele cha fasihi simulizi – mfano kuna Bi Msimulizi kuna hadhira. Pia kuna
"BI MSIMULIZI; Hadithi hadithi
HADHIRA; hadithi njoo!
Mwisho msimilizi anamalizia kwa kuuliza hadhira. "BI MSIMULIZI; niendelee nisiendeleee HADITHI YANGU IMEKWISHA
Pia kuna matumizi ya nyimbo, Bi moja anapagia jukwaani anaambatana na wimbo. Na mwisho wa tamthiliya inamalizika na nyimbo.
"Mkarara; nguzo mama, nguzo mama
Tukupambaje maua Tukupambaje maua"
Pia mwandishi ametumia nafsi mbalimbali
"BI MSIMULIZI; Kwa vile chizi kakimbia
Hadithi tamalizia Wakainua wakainua Siku ya kwanza ikapita.....
Ili kuuboresha mtindo mwandishi ametumia chizi ambaye ni mtu mwenye matatizo ya akili. Lakini ametumia kusema maneno yenye ukweli na uhalisia katika kazi yake.
"CHIZI: Wananiita mimi chizi
Chizi mie au nyie
Ambao macho mwakodoa Kuwachia wacheke
Wanavyotaka kufanya"
Kuandika majina ya wahusika wote kwa herufi kubwa. Jambo hili linamsaidia msomaji kufuatilia kazi ya mwandishi kwa urahisi.
"Bi MOJA; tena maneno yako yanatutia uvivu kabisa.
BI NANE; bila umoja hatutafanikiwa kitu"
Mwandishi ametumia mbinu ya kuweka picha katika jalada inayoonesha wanawake wakiinua NGUZO MAMA, ambayo pia ni mwanamke. Picha inasadifu yaliyomo kwani inaonesha harakati za kina mama zilivyoshindwa kuwa NGUZO MAMA.
Matumizi ya Lugha
Mwandishi ametumia lugha fasaha na inayoeleweka iliyojaa matumizi ya nahau, misemo, na tamathali za semi pamoja na mbinu za kisanaa.
- Nahau/ misemo Mfano: utakufa kibudu"
"Dume Malaya si dume roho yako kusumbua" "Utakiona cha mtemakuni"
"Watoto ni taifa la kesho"
"Akachanganya ulimi"
- Methali
Mfano: "asiye na mwana aeleke jiwe"
"Umoja ni nguvu utengano ni uadhaifu"
Taswira
Kuna taswira ya NGUZO MAMA ambayo inaonesha haki za wanawake
"BI MOJA: lakini kweli bila shaka tukivuta itasimama hii NGUZO MAMA
Jembe – kuachiwa mkulima
Kama – mbinu za kuinua NGUZO MAMA Mana - viti vizuri
Tamaathali za semi:-
- Tashbiha
"Amevaa kama mkulima wa bara" "Wanamwagwa kama mbuzi" "Anatembea kama kapigwaumbuwazi"
- Tashihisi
"Hasira zikampanda Bi Nane"
- Sitiari
"Mbwa mume wako, anayefuata wanawake ovyo" "Mie breki mie jeki"
Mbinu nyingine
- Takriri
"Wakajaribu wakajaribu" "Wakaenda wakaenda wakaenda"
- Mdokezo
"Wakavuta wakavuta"
"Hebu tutazame kwanza kwanini hawasogei."
- Tanakari sauti
Kigelegele
" Lu lu lu lu lu lu lu lu !
- Mjalizo
"Wakazaliana wakaongezeka" "Mvi, wakavu, vipara"
- Matumizi ya lugha ya matusi
"Malaya mkubwa wewe" "mbwa wee"
". mshenzi mkubwa"
- Lugha ya sauti ya kishairi
"CHIZI: Sikilizeni na sauti
Kama ndege wa nyikani Lakini moja sitaki
Msinitazame usoni Mama yangu kanizaa Sura langu baya baya Lakini mwenyewe mama Kwa hakika ni mzuri Baba yangu simjui Mama hataki nambia
- Matumizi ya kingereza
"My God"
Wahusika
- Bi Nane
Alichangia kwa kiasi kikubwa kuonesha dhana ya ukombozi wa mwanamke, Ni mwanamke msomi mwenye ushirikiano, alipenda kuwaelimisha wenzake. Mvumilivu na asiyekata tamaa, hakuwa na chuki wala hasira na hakupenda kulipa kisasi, Anafaa kuigwa.
- Bi Nne
Ni mpiga majungu anawivu mbinafsi mwenye chuki mwenye dhana potofu, Amechangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha juhudi za kuinua NGUZO MAMA, anatumia madaraka vibaya na hakuwa na elimu ya kutosha. Hafai kuigwa na jamii.
- Mwenyekiti
Mpenda fitina na mpika majungu anachukia wanawake anatumia madaraka yake vibaya. Ni kielelezo cha viongozi wasiokuwa na elimu ya kutosha. Hafai kuingwa na jamii.
- Bi Msimulizi
Huyu ndiye msimulizi wa matukio yaliyotendwa na wahusika mbalimbali, Ametumiwa kuuboresha mtindo hasa vipengele vya fasihi simulizi.
- Chizi
Mpenda demokrasia, Alipiga vita tabia ya uongo, Msema ukweli na mfichua maovu yaliyo katika jamii anaonyesha waziwazi sababu zilizosababisha wanawake wakashindwa kujikomboa.
- Bi. Moja
Mpenda anasa, Mke wa shabani. Ni mzembe hakuwa na msimamo katika kusimamia NGUZO MAMA. Anawakilisha wanawake, mwanamke anaependa kujipamba na kusahau maendeleo. Hafai kuigwa.
- Bi Pili
Ni mke wa sudi aliyenyanyaswa sana na mume wake. Ni mvumilivu hakuwa na elimu ni mlezi mzuri wa familia anafaa kuigwa.
- Bi Tatu
Mpenda starehe hana ushirikiano na wenzake hapendi kazi zisizokuwa na mshahara ni kielelezo cha wanawake wengi wanaokubali kuwa watumwa kwa kubembeleza wanaume zao kwa kuogopa kuachwa, Hafai kuigwa.
- Bi Tano
Ni mke wa maganga mwenye hasira anapenda anasa. Hakumpenda Bi Sita kwa sababu alimchukulia mume wake anafaa kuigwa na hafai kuigwa, Anakata Tamaa mapema.
- Bi Sita
Ni kahaba anatembea na waume za watu, mkorofi na mwenye matusi. Hapendi ushirikiano na wanawake wenzake, Anapenda starehe kuliko kazi, Hafai kuigwa kabisa.
- Bi Saba
Ni kiwakilishi cha wajane wanaoonewa katika masuala ya mirathi ni mlezi wa watoto aliyenyang'anywa kila kitu pamoja na watoto.Hafai kuigwa.
- Sudi
Mume wa Bi Pili mlevi na mvivu kiwakilishi cha wanaume wenye tabia ya kunyanyasa wake zao, Hafai kuigwa.
- Maganga
Mume wa Bi Tano si mwaminifu katika ndoa yake ni kielelezo cha wanaume wahuni, Hafai kuigwa.
Pia kuna wahusika wengine kama vile msichana ambaye ni kiwakilishi cha vijana, Pia Totolo, shaba kiando, makange, la mgambo.
Mandhari
Madhari ni ya kubuni lakini inayosawiri kwa kiasi kikubwa maisha ya vijijini na kwa kiasi Fulani maisha ya mjini, Mfano kilabuni, uwanjani, nyumbani ambamo zinauwezo kuwa mjini au vijijini. Pia uwepo wa vitu kama vile benz, Volvo na Bi Tatu kwenda kwenye pati inaashiria madhari ya mjini, Ngoma za madogori, Bi Pili kuwa mkulima, vilabu vya pombe vya mataputapu madhari ya kijijini.
Unyanyasaji na ugandamizaji wa wanawake ulionyesha madhari ya nchi yoyote ya kiafrika ambako kuna matatizo haya kwa kiasi kikubwa.
Jina la Kitabu
Jina la kitabu ni "NGUZO MAMA"ambayo kimejengwa kitaalamu na kinaisadifu vizuri yaliyomo ndani. Tamthiliya hii inaonesha harakati za wanawake wakiungana kwa pamoja kuunganisha umoja wao ili kupata maendeleo. Lakini harakati hizo zinakwama kutokana na matatizo kama majungu, fitina, na kutokuelewana.
Kimaudhui: Amefaulu kuonesha matatizo mbalimbali yanayowakumba wanawake wa kiafrika na vikwazo wanavyokabiliana navyo katika kutafuta ukombozi wa kweli.
Kifani: Mwandishi ametumia lugha rahisi inayoeleweka ya kishairi mafumbo rahisi na nyimbo zinazosababisha hivyo kufanya mchezo usichoshe. Pia inawajenga wahusika wake vizuri kwa kuwafanya waonekane wenye uhalisia na hivyo kubeba mawazo yanayosaidia hali halisi katika jamii.
Kimaudhui: Ameshindwa kuonyesha hatima ya wanawake wa Patata na jamii nzima baada ya kushindwa kuinua NGUZO MAMA.
Kifani: Kuna matumizi ya lugha ya matusi kwa mujibu wa maadili ya jamii yetu, lugha hii ni lugha isiyofaa.
Mwalimu
Unasoma somo hili? Niulize nikuelezee chochote kilichomo.
Ingia ili kumuuliza Mwalimu wa AI wa Sonza kuhusu mada hii.
Ingia ili kuuliza