Sonzaschool
Rudi

Msingi · Darasa la Saba

Kiswahili

Ngonjera

takriban dakika 2 kusoma

Mada za sehemu hiiTenzi Na NgonjeraMada 2
  1. Tenzi
  2. Ngonjera

Ngonjera

Ngonjera ni aina ya mashairi ya majibizano baina ya watu wawili au zaidi. Muundo wa ngonjera hufanana kabisa na mashairi.

Kwa kawaida, mijadala inayopatikana katika ngonjera huwa na malumbano yenye lengo la kutoa ujumbe maalumu kwa hadhira au jamii husika. Msemaji mmoja huuliza swali katika ubeti mmoja, kisha mwingine hutoa jibu katika ubeti unaofuata. Hivyo, majibizano ya hoja huendelea hadi mada husika inakamilika.

Tofauti na mashairi mengine au nyimbo, ngonjera haziimbwi bali husemwa. Mara nyingi, mada inayojadiliwa huibua utata kwa mhusika mmoja, ambaye kisha hupata ufafanuzi kutoka kwa mhusika mwingine.

Ngonjera: Vitendawili

Karimu

Nimepita kila kona, watu wengi wasifia, Wazee pia vijana, wengi nimewasikia, Wote wahamasishana, vitendawili sifia.

Rahimu

Karimu wewe Karimu, unatania hakika, Wakubwa nao watoto, wote wanajua fika, Vitendawili ni joto, la akili kutumika, Hutufanya kufikiri, jibu tunapotafuta.

Karimu

Nijulisheni kwa mifano, jinsi vilivyo muhimu, Nitakuunga mkono, ukinijaza elimu, Vitatu au vitano, vyatosha toa hukumu, Vitendawili kutega, faida yake ni nini?

Rahimu

Kwanza ni kufikirisha, tunapodaiwa jibu, Pili vinatufundisha, kuyakwepa masahibu, Mazingira vyahusisha, tuyajue kwa karibu, Ni nyingi faida zake, vitendawili kutega.

Karimu

Nimekutaka mifano, wewe wanipa faida, Wacha nikupe kibano, uache kupindapinda, "Chauma bila ya meno", tegua toa faida, Vitendawili kutega, faida yake siioni.

Rahimu

Jawabu lake ni moto, twatumia kila siku, Kulifikiria jibu, akili nimetumia, Moto vitu waharibu, pasipo meno tumia, Tahadhari tunapewa, tuutumiapo moto.

Karimu

"Ala lakini hashibi", jibu na funzo nataka, Leo ninapiga kambi, uniondolee shaka, Sitalitimua vumbi, hadi tupate mwafaka, Vitendawili kutega, sioni faida yake.

Rahimu

Ala lakini hashibi, jibu lake ni mauti, Nami ninapiga kambi, hadi tufike tamati, Hata tumwombe Yarabi, yatatufika mauti, Twafundishwa tutambue, kifo kwetu hakikomi.

Karimu

Leo Karimu nakiri, Rahimu wewe mwalimu, Tangu nianze kufikiri, nilibaki kulaumu, Sikutaka kuamini, bila kujua umuhimu, Vitendawili kutega, faida nimezijua.

Rahimu

Waungwana karibuni, tutegue na kutega, Nyumbani pia shuleni, vitendawili kutega, Mafunzo tuyapateni, uwezo tutaujenga, Ni nyingi faida kwetu, vitendawili kutega.

Swali

Katika ngonjera, jibu la swali hupewa na nani?

Ingia ili kuwasilisha jibu lako na lihesabiwe katika umahiri wako.

Ingia ili kufanya mazoezi

Mwalimu

Umekwama? Niulize chochote kuhusu mada hii.

Ingia ili kumuuliza Mwalimu wa AI wa Sonza kuhusu swali hili.

Ingia ili kuuliza