Mada za sehemu hiiKuchambua visababishi vya mabadiliko ya sera ya mambo ya nje na uhusiano wa kimataifaMada 3
- Kueleza chimbuko na misingi ya Sera ya mambo ya nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
- Kujadili mabadiliko ya Sera ya mambo ya nje na uhusiano wa kimataifa tangu 1964
- Kuchambua nafasi ya Sera ya mambo ya nje na uhusiano wa kimataifa katika kudumisha na kulinda maadili ya Kitanzania
Sera ya Mambo ya Nje ni mwelekeo rasmi unaobainisha msimamo na maamuzi ya taifa kuhusu uhusiano wake na mataifa mengine katika kuratibu masuala mbalimbali ya kimataifa.
Kila nchi duniani huwa na Sera ya Mambo ya Nje, ingawa chimbuko na misingi ya sera hizo hutofautiana kulingana na historia ya nchi husika, falsafa za uongozi, malengo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii, pamoja na muktadha wa kimataifa na kikanda.
Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania inalenga kulinda usalama na maslahi ya taifa, kukuza uchumi kupitia biashara na uwekezaji wa kimataifa, kutetea maslahi ya kisiasa na kiitikadi, kujenga hadhi ya taifa katika medani za kimataifa, pamoja na kukuza mshikamano wa kikanda na kimataifa.
Utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje unahusisha wadau mbalimbali: Rais ndiye mwenye mamlaka ya juu katika kufanya maamuzi ya kisera, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ikisimamia shughuli za kidiplomasia, Bunge hushiriki katika kujadili na kupitisha mikataba ya kimataifa, na vyombo vya ulinzi na usalama hushirikishwa ili kuhakikisha usalama wa taifa.
Chimbuko la Sera ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linahusiana moja kwa moja na hali ya kisiasa, kijamii na kiuchumi ya taifa jipya la Tanganyika, na baadaye Zanzibar, sambamba na mazingira ya kimataifa wakati nchi hizo zilipopata uhuru na baadaye kuungana.
1. Uhuru wa Tanganyika
Mara baada ya kupata uhuru tarehe 9 Desemba 1961, Tanganyika ilipata mamlaka kamili ya kuendesha sera zake za mambo ya nje kama taifa huru. Kabla ya hapo, masuala yote ya mambo ya nje yalikuwa chini ya usimamizi wa Serikali ya Uingereza.
Kupatikana kwa uhuru kuliwezesha Tanganyika kuanzisha balozi zake nje ya nchi, kujiunga na mashirika ya kimataifa kama Umoja wa Mataifa, na kushiriki kikamilifu katika mijadala ya kimataifa kwa mara ya kwanza kama mhusika huru. Katika hatua hiyo ya awali, Tanganyika ilikabiliwa na hitaji la dharura la kujitambulisha kimataifa kwa kuonesha taswira ya taifa la amani, lenye maadili na malengo ya maendeleo.
2. Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar
Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964 yalikuwa na mchango mkubwa katika kuunda na kuendeleza Sera ya Mambo ya Nje. Mapinduzi haya yaliondoa utawala wa Sultani na kuanzisha serikali ya watu wote chini ya uongozi wa Sheikh Abeid Amani Karume.
Serikali mpya ya Mapinduzi ya Zanzibar ilianzisha uhusiano wa karibu na mataifa ya Kisoshialisti kama China, Umoja wa Kisovieti (USSR), Cuba na Ujerumani Mashariki. Hatua hii iliibua mtazamo mpya wa kidiplomasia katika ukanda wa Afrika Mashariki.
3. Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, uliunda taifa jipya lenye dira na msimampo mipya ya kidiplomasia.
Tanganyika ilipoingia katika Muungano, tayari ilikuwa na misingi ya sera ya mambo ya nje iliyojikita katika kutofungamana na upande wowote (Non-Aligned Movement), mshikamano wa Afrika na diplomasia ya kimaadili chini ya uongozi wa Mwl. Julius Kambarage Nyerere. Zanzibar, kwa upande wake, baada ya mapinduzi ilikuwa na msimamo wa kijamaa na uhusiano wa karibu na mataifa ya Kisoshialisti.
Muungano wa pande hizi mbili uliwalazimisha viongozi wa taifa jipya kuunda sera ya mambo ya nje iliyoweza kuunganisha na kuakisi msimamo ya pande zote mbili.
4. Vuguvugu la Ukombozi Barani Afrika
Vuguvugu la ukombozi barani Afrika lilikuwa chanzo muhimu cha Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania, kwa kuwa katika kipindi hicho mataifa mengi ya Afrika bado yalikuwa chini ya utawala wa kikoloni na mifumo ya ubaguzi wa rangi.
Mara baada ya kupata uhuru, Tanzania ilijitokeza kama kimbilio la wapigania uhuru kutoka nchi mbalimbali kama Msumbiji, Zimbabwe, Afrika Kusini na Namibia. Kupitia falsafa na uongozi wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Tanzania ilichukua msimamo wa kidiplomasia uliotegemea haki, utu na usawa wa binadamu.
Harakati za ukombozi katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara ziliratibiwa jijini Dar es Salaam kupitia Kamati ya Ukombozi ya Umoja wa Afrika, ikiongozwa na Brigedia Jenerali Hashim Mbita.
5. Vita Baridi
Tanzania ilipata uhuru wakati dunia ikiwa imegawanyika katika kambi mbili za kiitikadi: Mashariki chini ya Muungano wa Kisovieti na Magharibi chini ya Marekani.
Katika muktadha huo, Tanzania ilichagua sera ya kutofungamana na upande wowote ili kulinda uhuru wa maamuzi yake ya kisera na kidiplomasia. Msimamo huu ulijidhihirisha, kwa mfano, katika ujenzi wa reli ya Tanzania–Zambia (TAZARA) iliyofadhiliwa na China, pamoja na misaada ya maendeleo kutoka nchi za Skandinavia na Benki ya Dunia.
6. Maadili ya Ujamaa
Maadili ya Ujamaa yalikuwa msingi muhimu wa Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania baada ya uhuru, kwa kuwa yalisisitiza usawa, mshikamano na kuthamini utu wa binadamu.
Kupitia msingi hii, Tanzania ilipiga ukoloni na ukoloni mamboleo kwa kusaidia mataifa ya Kiafrika yaliyokuwa bado hayajapata uhuru, iliunga mkono mshikamano wa Afrika na nchi za Dunia ya Tatu kupitia Umoja wa Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM).
Misingi ya Sera ya Mambo ya Nje ni kanuni kuu, maadili na mwelekeo unaoongoza namna Tanzania inavyowasiliana, kushirikiana na kujenga uhusiano na mataifa mengine. Katika kipindi cha awali baada ya uhuru, Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania ilijengwa juu ya misingi mitano ifuatayo:
1. Amani na Ujirani Mwema
Huu ulikuwa msingi muhimu wa Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania mara baada ya uhuru. Taifa changa lilihitaji mazingira ya utulivu ili kujenga maendeleo ya ndani na kuimarisha heshima yake kimataifa.
Kupitia sera hii, Tanzania ilijenga uhusiano wa kirafiki na nchi jirani kama Kenya, Uganda na Msumbiji, na ikahamasisha mazungumzo na ushirikiano wa kikanda. Aidha, Tanzania ilichukua msimamo wa kidiplomasia katika kuzuia migogoro ya mipaka na kuunga mkono misingi ya Umoja wa Nchi za Afrika (OAU) iliyositiza kuheshimu mipaka ya kikoloni.
2. Umajumui wa Kiafrika
Huu ulikuwa msingi mkuu wa Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania baada ya uhuru. Falsafa ya umajumui wa Kiafrika ilisitiza mshikamano na ushirikiano wa Waafrika kama njia ya kuondoa ukoloni na kuimarisha maendeleo ya bara.
Mara baada ya Tanganyika kupata uhuru, sera ya mambo ya nje iliweka kipaumbele katika kuunga mkono uhuru wa mataifa yaliyokuwa bado chini ya ukoloni na kupinga ubaguzi wa rangi. Tanzania ilishirikiana kwa karibu na mataifa mengine ya Afrika katika harakati hizi na mwaka 1963 ikawa miongoni mwa waanzilishi wa OAU mjini Addis Ababa.
3. Kutofungamana na Upande Wowote
Kutofungamana na upande wowote ulikuwa msingi muhimu wa sera ya mambo ya nje ya Tanzania kutokana na mazingira ya Vita Baridi yaliyogawanya dunia katika kambi mbili kuu.
Tanzania iliamua kutoegemea upande wowote ili kulinda uhuru wake wa maamuzi na kuepuka kugeuzwa chombo cha mataifa makubwa. Kupitia msimamo huu, Tanzania iliweza kushirikiana na pande zote mbili na kunufaika na misaada ya maendeleo bila kufungwa na itikadi za kambi yoyote.
4. Kusaidia Ukombozi wa Afrika
Kusaidia harakati za ukombozi ulikuwa msingi muhimu wa sera ya mambo ya nje ya Tanzania, kwani taifa hili changa lilijitambulisha kama ngome ya kupinga ukoloni na ubaguzi wa rangi barani Afrika.
Baada ya Tanganyika kupata uhuru mwaka 1961, Mwalimu Julius K. Nyerere alisitiza kuwa uhuru wa Tanganyika hauna maana iwapo mataifa mengine ya Afrika bado yapo chini ya ukoloni. Kwa msingi hiyo, Tanzania ilitoa msaada wa moja kwa moja kwa wapigania uhuru kutoka nchi za Kusini mwa Afrika kama Afrika Kusini, Zimbabwe, Msumbiji na Namibia.
5. Maadili, Ujamaa na Haki za Binadamu
Katika msingi huu wa Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania, falsafa ya Ujamaa iliyosisitiza mshikamano, usawa na utu wa binadamu iliunganishwa na mweleo wa kidiplomasia wa taifa.
Tanzania ilisisitiza usawa wa mataifa yote, ikapinga ukoloni na ukoloni mamboleo, na ikaunga mkono uhuru wa kisiasa kwa nchi zilizokuwa bado chini ya tawala za kikoloni. Maadili ya haki za binadamu yaliifanya Tanzania kuchukua msimamo wa kidiplomasia wa kupinga dhuluma, uonevu na ubaguzi.
Kujua chimbuko na misingi ya Sera ya Mambo ya Nje kunasaidia kuelewa kwa nini Tanzania inashirikiana na nchi fulani kulingana na historia na maadili ya taifa. Kwa mfano, unaposoma habari za Tanzania ikitoa msaada wa kibinadamu kwa nchi inayokabiliwa na vita au msumbiji, unaweza kuelewa kwamba sera hiyo inatokana na msingi wa amani na ukombozi ulioanzishwa tangu uhuru. Pia, unapogundua kuwa Tanzania inashiriki katika mashirika ya kikanda kama EAC na SADC, unaweza kuhusisha hayo na misingi ya umajumui wa Kiafrika ulioanzishwa miaka ya 1960.
Swali
Chimbuko kuu cha Sera ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni upatikanaji wa:
**Choice: **
Ingia ili kuwasilisha jibu lako na lihesabiwe katika umahiri wako.
Ingia ili kufanya mazoeziMwalimu
Umekwama? Niulize chochote kuhusu mada hii.
Ingia ili kumuuliza Mwalimu wa AI wa Sonza kuhusu swali hili.
Ingia ili kuuliza